Hakielimu yazindua Mpango Mkakati wa miaka mitano - MUANGALIZI

Hot

Post Top Ad

Your Ad Spot

Thursday, January 19, 2017

Hakielimu yazindua Mpango Mkakati wa miaka mitano

 Na Mwandishi Wetu

Mhandiri wa Chuo kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Kitillya Mkumbuko akizungumza na wadau wa elimu katika moja ya mikutano ya hakielimu

BALOZI wa Sweden Nchini Tanzania Katrina Rangnitt amezindua mpango mkakati wa  miaka mitano  2017/2021 wa Taasisi isiyokuwa ya kiserikali ya Haki Elimu unaojikita katika uboreshaji elimu nchini Tanzania.
Akizindua mpango huo balozi wa Sweden  Rangnitt kwa kushirikiana na  bodi ya taasisi hiyo, alisema kuwa mkakati huo ni kufanya ushawishi kwa serikali  ili iandae na kutekeleza sera ambazo zitakuwa fursa kwa watoto hususani katika kuandikishwa shule, usawa wa elimu jumuishi iliyo bora, inayotolewa kwenye mazingira rafiki na salama kwa wote.
Pia alisema mkakati huo utahakikisha kuwa wananchi wanapata taarifa, wanajipanga kwa  kushiriki katika kutatua changamoto zilizopo katika shule nyingi nchini hususani kwa kufuatilia utawala na utoaji elimu bora.
Kwa upande wake Mkurugenzi mtendaji wa Haki Elimu John Kalage, alisema kuwa mkakati huu wa  miaka mitano ni kuhakikisha  wanashawishi mabadiliko ya  sera na utekelezaji wake.
Alisema elimu ya Tanzania haina falsafa iliyo  wazi hivyo inashindwa kufiki ujumuishaji kamili wa makundi yote na kutoa  matokeo bora ya kujifunza  yenye manufaa kwa wanafunzi.
"Shule  si sehemu salama kwani mtoto mmoja kati ya wawili hukumbana na ukatili ambao umezoeleka kutendwa na walimu hivyo kuna haja ya  kufanya marekebisho zaidi sera ya elimu na kampeni ya kuhimiza utekelezaji makini wa sera ya elimu ya mwaka 2014 ili kuhakikisha upatikanaji wa elimu na ubora wake vinaimarika,"alisema Kallage.
Alisema licha ya juhudi za serikali  zinazoendelea, sekta ya elimu nchini Tanzania bado imesongwa na  changamoto kubwa ambazo ni pamoja na  matokeo duni ya ufundishaji wa wanafunzi, utoro wa Waalimu na uwezo mdogo wa kufundisha na kukosekana kwa  usawa wa kijinsia.
Pia alisema  kushamiri kwa  mfumo tabaka wa elimu ni tatizo kwani watoto wa wenye fedha wachache wanapata elimu bora kwenye shule binafsi na masikini wanaachwa kwenye elimu duni katika shule za serikali.
Aliongeza kuwa kukosekana kwa falsafa na malengo ya elimu vinavyoeleweka kwa kila mtu matokeo yake, elimu ya Tanzania imekosa falsafa na malengo ya kuiongoza.
Naye Mhadhiri wa Chuo kikuu cha Dar es Salaam Profesa Kitillya Mkumbo,alisema serikali inatakiwa kuchukua hatua za muda mfupi za kutatua changamoto za elimu ya msingi kutokana na mfumo ambao siyo bora.
Pia alisema Mtazamo wa serikali kwa vyuo vya ufundi bado msukumo wake ni mdogo, hivyo wanatakiwa kuelekeza nguvu katika vyuo hivyo ili kupata watu wenye ujuzi na kufikia lengo la kuwa na serikali ya viwanda.
Vile vile alisema elimu ya juu hapa nchini  inawalimu wachache  wenye shahada ya uzamivu ambapo ni asilimia 25 tu na chuo Kikuu cha Dar es Salaam ndiyo wenye  walimu wengi wenye shahada hizo  hivyo kuna haja ya  serikali kuwekeza kwenye elimu na kutoa elimu bora.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot