Kiiza aitolea Uvivu Simba - MUANGALIZI

Hot

Post Top Ad

Your Ad Spot

Sunday, July 24, 2016

Kiiza aitolea Uvivu Simba

Mshambuliaji aliyetupiwa vilago na klabu ya Simba, Hamis Kiiza akishangilia moja ya bao aliloshinda kwenye ligi kuu ya vodacom katika moja kati ya mechi alizochezea timu hiyo.
Na Mwandishi Wetu

MSHAMBULIAJI aliyetupiwa virago na klabu ya Simba, Hamisi Kiiza amesema timu hiyo haiwezi kupata mafanikio hata kama itasajili wachezaji wote nyota wanaotamba kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara.

Nyota huyo raia wa Uganda, amekwenda mbali zaidi akisema hata kama Simba ikimsajili Mtanzania Mbwana Samatta anayecheza KRC Genk iliyopo Ligi Kuu ya Ubelgiji haitakuwa na mafanikio hadi baadhi ya viongozi ambao hakutaka kuwataja waondoke madarakani.

Kiiza ameenguliwa kwenye kikosi cha msimu ujao wa Ligi Kuu na uongozi wa timu hiyo, licha ya kushika nafasi ya pili kwa ufungaji bora kwa kufunga mabao 19, kwenye mechi za Ligi Kuu Tanzania Bara msimu uliopita.

Akizungumza na Blogu hii kwa njia ya mtandao, Kiiza aliyepo kwao Uganda akisaka timu ya kuichezea msimu ujao, alisema tatizo kubwa la Simba ni uongozi na siyo wachezaji wala makocha ambao wamekuwa wakibadilishwa kila msimu.
 
“Sidhani kama kutakuwa na mabadiliko hata kama wakiwasajili wachezaji wote wanaofanya vizuri Tanzania, wamrudishe na Mbwana Samatta, tatizo kubwa lililopo Simba ni baadhi ya viongozi ambao wamekuwa na chuki na wachezaji hasa anaposema ukweli na kudai haki zake,” alisema Kiiza.

Mshambuliaji huyo wa zamani wa Yanga, alisema ameshindwa kumalizia mkataba wake wa mwaka mmoja uliobaki Simba kwa sababu ya tuhuma mbalimbali zilizokuwa zikimkabili ndani ya timu hiyo, kubwa ikiwa ni kuambiwa anaigawa timu na kwamba ana mapenzi na Yanga.


Mshambuliaji aliyetupiwa vilago na klabu ya Simba, Hamis Kiiza akisalimiana na Kocha Mkuu wa Timu ya Yanga Hans Van Pluijm katika moja kati ya mechi iliyozikutanisha timu hizo mbili za watani wa jadi.

Alisema kama angekuwa anaihujumu timu hiyo asingefunga mabao kwa idadi kubwa kwa sababu asilimia kubwa ya mabao aliyofunga ndiyo yameipa ushindi timu hiyo, hadi kuna wakati ikawa inaongoza ligi na kuziacha mbali Yanga na Azam.

Alisema Simba ilikuwa na nafasi kubwa ya kubeba ubingwa msimu uliopita, lakini fitna za baadhi ya viongozi hao ndiyo ziliwaumiza na kwamba walikuwa na nafasi kubwa tangu wakiwa na kocha Dylan Kerr na Jackson Mayanja.


 Mshambuliaji wa Zamani wa Timu ya Yanga, Hamis Kiiza akigombea mpira dhidi ya beki wa timu ya Azam Gadiel Michael(Kulia)
Akizungumzia tuhuma hizo, Mwenyekiti wa kamati ya usajili ya Simba, Zakaria Hanspoppe alisema benchi lake la ufundi halikuona sababu ya kuendelea na mchezaji huyo kutokana na kutokuwa na sifa, ikiwemo utovu wa nidhamu.

Kiiza anadaiwa kuhamasisha migogoro kwenye timu, ikiwemo lile sakata la wachezaji wa kigeni kugoma kwenda Songea kwenye mechi ya mwisho ya ligi wakishinikiza kulipwa mishahara yao.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot